Kwa uzoefu wangu wa ukulima na ufugaji wa asili, na hata wataalam wanathibitisha hili, sungura ni mnyama rahisi wa kufuga kwani hana gharama kubwa na ndiyo maana shughuli hii inaweza kufanywa na mkulima mdogo asiye na mtaji mkubwa.
Chakula cha sungura ni kama nyasi, mboga kama vile sukuma, spinachi, kabichi, karoti, mchunga na pia unaweza kununua chakula halisi cha sungura kutoka maduka ya vifaa vya wanyama.
Sungura akila vyakula hivi vibichi anakojoa mara kwa mara, na nilivyodokeza katika makala iliyotangulia, mkojo wake ni mali unaweza kukuleta kipato kikubwa kwa sababu unatumika katika maabara.
Hata hivyo, kama unataka kumkinga na magonjwa ya tumbo, unashauriwa kukausha chakula chake, jambo ambalo pia husaidia asikojoe hovyo.
Kama nilivyoeleza hapo awali, kila kizimba cha sungura lazima kiwe na eneo ama chombo cha kuwekea chakula, tena unaweza kuongeza chemba maalumu kwa ajili ya kuwekea nyasi.
Chemba hiyo ni vyema iwe na nyasi maalumu kila wakati – na wataalamu wa ufugaji sungura wanapendekeza majani aina ya Alfalfa, lakini kama unapata majani ya mchunga ni mazuri sana kwa sababu hawa jamaa wanayapenda mno kwani yana viinilishe vingi.
Sungura wanakula vyema nyasi zikiwa zimekatwa katwa katika kipimo cha inchi tatu au nne. Kusanya kitita cha majani na ukikate kwa panga kwa urefu huo.
Unaweza pia kumlisha sungura wako mikundekunde na jamii yake, kabichi, spinachi na Sukuma wiki. Usisahau kwamba wanakula pia mizizi na ikiwa karoti zinapatikana wapatie.
Hata hivyo, hakikisha unaondoa mabaki yote ya chakula ambacho wameshindwa kula. Ondoa kila siku kwenye kizimba na baada ya muda utagundua wanapendelea nini zaidi, kwa sababu unaweza usikute mabaki.
Walishe sungura wako mboga mboga kwa taratibu kama hawajazowea mpaka watakapokuwa wamezowea. Wakati mwingine wakil asana wanavimbiwa au hupata ugonjwa wa kuhara.
Pia uwalishe vyakula maalumu vya sungura vinanvyopatikana kwenye maduka ya vyakula vya mifugo. Unaweza kuwalisha hata njugu mawe kwa sababu wanazipenda pia.
Unaweza kupata mwongozo wa awali hata kwa mtu ambaye amekuuzia sungura hao namna anavyowalisha, lakini kama kuna ofisa ugani karibu yako, mtumie ili akuelekeze vyema. Sungura mmoja mkubwa huweza kula chakula kiasi cha gram 100 had 130 kwa siku nahii ni kwa chakula chake maalumu special kwa sungura. Pamoja na chakula cha ziada kama vile majani mabichi majani makavu nk.
MFANO WA MCHANGANUO WA CHAKULA BORA CHA SUNGURA
Namba | AINA YA CHAKULA | KIASI |
1 | Pumba za Mahindi | 40kg |
2 | Mashudu ya Alizeti | 30kg |
3 | Pumba za Mpunga | 15kg |
4 | Soya | 5kg |
6 | Chumvi | 0.5kg |