Katika toleo liliotangulia, tulizungumzia kuhusu utayarishaji wa mabwawa na
matangi ya kufugia kambare, muda na kiasi cha mbolea na chokaa kinachohitajika kuongezwa kabla ya kuingiza samaki, uchaguzi na usafirishaji wa vifaranga vya kambare. Katika toleo hili tunamalizia kwa kuangalia mambo muhimu ya kuzingatia kabla ya kuingiza vifaranga hivyo kwenye bwawa.

NAMNA YA KUWAINGIZA VIFARANGA KWENYE BWAWA
TARATIBU NA IDADI YA VIFARANGA
• Usimimine maji toka kwenye vyombo vya kusafirishia pamoja na vifaranga kwa sababu kwa kufanya hivyo utawathiri kiafya vifaranga.
• Kwanza mwaga kiasi cha theluthi moja ya maji kutoka kwenye chombo cha kusafirishia na ukijaze maji toka kwenye bwawa husika la samaki.
• Subiri kwa dakika tatu mpaka tano, halafu shusha chombo polepole kwa kuelekeza kwenye bwawa na mimina polepole huku ukichunguza kama kuna samaki yeyote aliyekufa wakati wa usafirishaji.
• Hakikisha kunakuwa na vifaranga kati ya 5 hadi 6 kwa kila mita moja ya mraba ya maji.
• Iwapo unataka wakue, wapunguze hadi kufikia nusu idadi yao baada ya miezi 6 na uendelee kuwalisha.
• Unaweza kujenga mabwawa kwa madhumuni mbalimbali kutegemeana na hali ya soko la samaki lilivyo au hatua
ambayo ungependa kuwauza samaki wako.
CHANGAMOTO ZA UFUGAJI KAMBARE NCHINI:
• Kutopatikana vifaranga wa kutosha unaosababishwa na kukosekana kwa miundominu ya kutosha kwa ajili ya utotoleshaji wake kwa kiwango cha biashara ukitilia maanani soko la kambare linazidi kukua nchini. Kuna haja ya serikali kupitia wizara husika kuwekeza vilivyo kwenye miundombinu na kuhamasisha wafugaji kujikita kwa lengo la kukidhi mahitaji ya soko la samaki nchini.
• Vilevile uwepo wa tatizo la kambare wakubwa kuwala wadogo, maadui wengine kama vile vyura, wadudu wa majini, wezi na ndege kama tai kuwala kambare. wafugaji wanashauriwa kutumia zana kama nyavu za mbu kuweza kufunika na kuzuia maadui hawa kuwala kambare au kuongeza samadi mara kwa mara bwawani ili kuzuia samaki wasionekane na kushambuliwa kirahisi na maadui.
• Ufugaji wa kambare nchini ni kama machimbo ya dhahabu yasiyochimbwa, kuna haja ya serikali yetu kujikita kikamilifu katika uwekezaji wake ili kuwahamasisha na kuwawezesha wananchi kuingia katika ufugaji huu ili kuzalisha chanzo hiki rahisi cha protini mbadala kwa matumizi yao na kujiongezea kipato zaidi